Art for Peace Submissions

Art for Peace Submissions

SHAIRI by Onyando Emmanuel Ochieng'

Published

May 16, 2026

Author

Sylvia Moraa

Organization

IPPNW

Msimulizi, kwa njia ya shairi anakumbuka vita vilivyotokea baada ya uchaguzi uliokuwa nchini. Yeye pamoja na wanawe wakiathirika moja kwa moja. Majumba yakiporomoshwa na kubakia vifusi huku milio ya risasi ikiendelea kusikika kwani vyeo vilikuwa viking’ang’aniwa. Vita hivi vikisababisha vifo na wengi kutoroka nchi yao. Anamalizia kwa kurai amani iimbe ili kusababisha utulivu na umoja.

 

 

                                   IMBA AMANI IMBA

 

 

Vilivyobakia ni vifusi,

Pengine wanangu wamo ndani,

Milio ya risasi ikisikika kwa mbali,

Kuwatafuta bado siachi,

Yananidondoka machozi,

Vumbi ikitawala hewani,

Bado ninalo tumaini,

Pengine kuwapata hai.

 

Mlichokileta tazama,

Wenye mioyo ya chuma,

Vyeo mking’ang’ania,

Nasi nyasi tunaumia,

Utulivu mmerarua,

Nchi yetu tunaitoroka,

Msielewane mbona?

Umoja kudumisha.

 

Nikichoka tayari,

Zinatufikia Habari,

Wengine wako hospitalini,

Na wengine mochari,

Ila wanawatibu nani?

Hawapo madaktari,

Vitanda vyao wamelalia,

Vifo vyao kusubiri.

 

Vilio, mingurumo ya huzuni,

Tokeo lake Izraili,

Tukiyakubali mauti,

Twapoteza tumaini,

Wanangu tena hawaamki,

Zimewatoka pumzi,

Hivi nielezeni,

Nitawahi kupona kweli?

 

 

 

Vile vitoto tazama,

Vilivyobaki yatima,

Kwa uchungu vinalia,

Kwenye miili ya wazazi,

Ya kwangu afadhali,

Hili lauma zaidi,

Nchi yangu jamani,

Kwani una nini?

 

Uwanjani, majeneza yamelandana,

Tumefika, miili kupokea,

Eti, wametufadhili hawa,

Waliotuletea hii tanzia,

Wanatuahidi fidia,

Ishara ya huruma,

Eti, wanatuombea,

Tupate kufarijika.

 

Hadi lini jamani?

Kila wakati ni hivi,

Historia hatujifunzi,

Au pengine hatujali,

Basi yatukumbushe makaburi,

Ya wetu wapenzi,

Linapotokea hili,

Tunaumia mioyoni.

 

Hiki mojawapo visa,

Nilichopitia,

Amani ikiondoka,

Haya twapitia,

Akili inanguruma,

Moyo hauna kimya,

Picha za kale twatazama,

Utulivu kutukumbusha.

 

Basi imba amani imba,

Sauti yako paza,

Kote nchini sikika,

Umoja himiza,

Chuki, ukabila ondoa,

Vita tamausha,

Usilale naomba,

Bendera yako peperusha.

 

 

 

 

 

 

Imba amani imba,

Hadi kwenye ndoa,

Watoto wasilale njaa,

Eti mama kaondoka,

Usaliti kemea,

Wakuogope wabaya,

Unafiki furusha,

Ukatili kanyaga.

 

 

 

Imba amani imba,

Kuchoka Hapana,

Utulivu leta,

Moyo uwe kimya,

Kwenye dini usiogope,

Ndipo sote tushikane,

Palipo amani,

Afya, uzima hapakosi.

 

 

 

                                                                     NA:

 

                                                                                  Onyando Emanuel Ochieng’

                                                                                   C3/1482/2024

                                                                                 emanuelonyando@students.uonbi.ac.ke 

                                                                                 emanuelochieng621@gmail.com 

                                                                                   0706760212